Katibu Tawala wa Mkoa wa Kilimanjaro, Bw. Kiseo Nzowa, ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Siha kwa mafanikio makubwa katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, hatua inayochochea kwa kiasi kikubwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo na uboreshaji wa huduma kwa wananchi wa wilaya hiyo.
Akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani cha kujadili hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Bw. Nzowa alisema kuwa juhudi madhubuti zinazofanywa na viongozi na watendaji wa Halmashauri hiyo katika kuhakikisha mapato yanakusanywa kwa ufanisi na uaminifu ni mfano bora unaopaswa kuigwa na halmashauri nyingine ndani ya Mkoa wa Kilimanjaro.
Aidha, amemuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Dkt. Haji Mnasi, kuendeleza juhudi hizo ili kuisaidia serikali kufanikisha ajenda ya maendeleo kwa wananchi wa Siha.
Katika hatua nyingine, Bw. Nzowa alitumia nafasi hiyo kuwasilisha taarifa rasmi ya kuhitimishwa kwa shughuli za Mabaraza ya Madiwani katika Halmashauri zote za Mkoa wa Kilimanjaro, kufuatia ukomo wa muda wa uongozi wa Madiwani waliopo. Alitoa wito kwa madiwani hao kuhakikisha wanarejesha vitendea kazi walivyokabidhiwa na halmashauri katika kipindi chao cha utumishi, ili viweze kutumika kwenye awamu ijayo.
Takwimu za hivi karibuni zinaonesha kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Siha imevuka lengo la ukusanyaji wa mapato ya ndani kwa zaidi ya asilimia 100, ikifikia asilimia 114 katika mwaka wa fedha 2024/2025..
17 Barabara ya Florida
Anuani ya Posta: P. O. Box 3070, Moshi
Simu: +255 (027) 2754236/7
Mobile:
Anuani pepe: ras@kilimanjaro.go.tz / ras.kilimanjaro@tamisemi.go.tz
Hakiimiliki©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Kilimanjaro.Haki zote zimehifadhiwa