Katibu Tawala wa Mkoa wa Kilimanjaro, Bw. Kiseo Nzowa, ametoa wito kwa Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Hai, Ndg. Bakarani Urio kuharakisha mchakato wa utoaji wa mikopo isiyo na riba kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu vilivyokidhi vigezo na masharti ya mikopo hiyo vipatiwe kabla ya mwaka wa fedha wa Serikali kuisha.
Akizungumza leo Juni 18,2025 katika kikao cha Baraza la Madiwani cha kujadili hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Bw. Nzowa alisema kuwa ni muhimu kwa Halmashauri kuhakikisha fedha za mikopo ya asilimia kumi ya mapato ya ndani zinatolewa kwa wakati kwa walengwa ndani ya mwaka huu wa fedha wa serikali 2024/2025 ili zikawasaidie Wananchi kufikia malengo yao ya kiuchumi.
Katika kikao hicho, Bw. Nzowa pia alilipongeza Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Hai kwa ushirikiano mzuri na timu ya wataalamu wa halmashauri katika kusimamia na kutekeleza miradi ya maendeleo kwa kasi na ufanisi.
Aidha, amezipongeza Halmashauri za Mkoa wa Kilimanjaro ambazo zimefanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, akiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Hai iliyofanikisha ukusanyaji wa mapato kwa asilimia 100 kwa mwaka wa fedha 2024/2025.
Pamoja na mafanikio hayo, Bw. Nzowa alitoa wito kwa halmashauri zilizofikia malengo ya mapato kuendelea kukusanya zaidi ili kuiwezesha serikali kuwa na fedha za kutosha kwa ajili ya kugharamia miradi mbalimbali ya maendeleo kwa wananchi.
17 Barabara ya Florida
Anuani ya Posta: P. O. Box 3070, Moshi
Simu: +255 (027) 2754236/7
Mobile:
Anuani pepe: ras@kilimanjaro.go.tz / ras.kilimanjaro@tamisemi.go.tz
Hakiimiliki©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Kilimanjaro.Haki zote zimehifadhiwa